-->

NDALICHAKO ACHARUKA, OFISA MANUNUZI MATATANI

Picha


VIFAA vya maabara vyenye thamani ya Sh milioni 759 vilivyonunuliwa mwaka 2016 kwa ajili ya Chuo cha ualimu wilayani Kasulu mkoani Kigoma, havijatumika kutokana na kuwa chini ya kiwango.
Aidha imebainika kwamba vifaa kama hivyo pia vipo katika vyuo vingine vinne.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako ameagiza kuchukuliwa hatua kwa watendaji wa Chuo cha Ualimu Kasulu na baadhi ya watendaji wa wizara yake kwa kufanya manunuzi ya vifaa vya maabara vilivyo chini ya kiwango.
Alisema kitendo cha watendaji hao ni uhalifu kama uhalifu mwingine na kutaka Katibu Mkuu wa wizara hiyo kuchukua hatua kali kwa wote waliohusika kununua na kupokea vifaa hivyo.
Pia alimtaka Katibu Mkuu huyo kumchunguza na kumchukulia hatua ofisa manunuzi wa wizara hiyo, Audfas Myonga kwa kuhusishwa na ununuzi na usambazaji wa vifaa hivyo katika vyuo vinne vya ualimu nchini.
Profesa Ndalichako alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na watumishi wa chuo hicho baada ya kutembelea bohari za kuhifadhia mali za chuo na kushuhudia vifaa hivyo vikiwa bado kutumika.
Mkufunzi wa masomo ya baolojia chuoni hapo, Joshua Yussuf alisema kuwa vifaa vingi vilivyopokewa vikiwa vimeletwa na kampuni ya Satima havijatumika kutokana na kutoendana na module za ufundishaji za chuo hicho.
Pamoja na maelezo hayo, Waziri Ndalichako aliuliza sababu ya chuo kuagiza vifaa ambavyo havina matumizi chuoni ambapo Boharia wa Chuo cha Ualimu Kasulu, Melkzedek Waziri alisema vifaa hivyo havikuagizwa na chuo bali walivipokea kwa maagizo ya watendaji kutoka wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Waziri Ndalichako katika mazungumzo hayo alimtaka Kaimu Mkurugenzi wa mafunzo ya Ualimu, Frederick Shuma kutoa ufafanuzi kuhusu jambo hilo ambaye alisema kuwa vifaa hivyo vilisambazwa kwa maombi ya mahitaji ya vyuo, jambo lililomkera Waziri na kutaka wale wote waliohusika na sakata hilo kuchukuliwa hatua. A
lisema kiasi hicho kikubwa cha fedha za serikali kutumika kununua vitu ambavyo havihitajiki, tena vikiwa vibovu na chini ya viwango haliwezi kuvumiliwa.
Waziri Ndalichako alisema ameshangazwa na chuo kupokea vifaa mwaka 2016 lakini hadi sasa bado viko kwenye maboksi wakati kiasi kikubwa cha fedha za serikali kimetumika fedha ambazo zingeweza kufanya shughuli nyingine za maendeleo.
Waziri huyo alitaka kupewa orodha ya vifaa vyote vilivyoletwa hapa chuoni, nyaraka za waliovileta, waliopokea hapa chuoni na mchakato mzima vilipotoka hadi kufika hapo.

Read also-: