-->

Katibu CWT awavaa walimu

CHAMA cha Walimu (CWT) Mkoa wa Arusha kimesema walimu wasiotambua wajibu wao wamekuwa wakichangia kuporomoka kwa ufaulu wa wanafunzi na kuporomoka kwa elimu.
Katibu wa chama hicho mkoani hapa, Veronica Mtalo, akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa CWT Taifa, Ezekiah Oluoch, alisema taifa linahitaji walimu wenye ufanisi wa hali ya juu ili kutoa elimu yenye manufaa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Alisema hayo wakati akifunga mafunzo kwa wakuu wa vyuo vya ualimu, walimu na wakufunzi wa masomo ya hesabu wilayani Monduli juzi.
Alisema walimu wasiojitambua wamekuwa wakichangia kushuka kwa ufaulu wa wanafunzi kutokana na kutotimiza wajibu wao ipasavyo.
“Walimu ni watu muhimu sana, hivyo wasipojitambua ni janga kwa taifa na natoa wito kwa walimu watumie taaluma yao vizuri kwa maendeleo ya elimu ya Tanzania.”
"Ni vizuri kila mwalimu akajiendeleza zaidi na kuachana na mitandao michafu na badala yake mjikite kwenye kutafuta mitandao yenye maendeleo ili muwe walimu bobezi," alisema.
Mtalo alisema baadhi ya walimu wameacha nafasi ya ulezi na kusababisha wanafunzi kuwa na mienendo isiyofaa.
“Mwalimu anatakiwa kufundisha kwa upendo, anatatakiwa kujiendeleza siku hadi siku, ila sababu wengi hatujitambui tunabaki kulia mshahara mdogo, hapana pamoja na mshahara mdogo jiongezeni zaidi ili muwe mwalimu wa kisasa,” alisema.
Naye meneja mradi wa uboreshaji wa elimu kwa shule za msingi, Donatian Marusu, alisema mradi wa kuelimisha walimu bobezi wa masomo ya hesabu una lengo la kuwafikia walimu wa shule zote mkoani hapa.

Read also-: