-->

Walimu waliopunguza umri kukatwa mafao


WALIMU wanaofanya udanganyifu katika taarifa zao za kiutumishi, kwa lengo la kujiongezea muda wa kuwepo kwenye utumishi wa umma, kuanzia sasa, watakapobainika, watakatwa mafao yao, kufidia mishahara yote waliyolipwa katika kipindi chote, walichojiongezea.
Hayo yalibainishwa na Katibu wa Ofisi ya Rais, Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC), Winifrida Rutahindurwa, mjini Bagamoyo jana alipokutana na walimu wakuu na wakuu wa shule za umma kutoka wilaya za Bagamoyo na Chalinze.
Lengo la mkutano wake huo, ilikuwa ni kutoa elimu juu ya wajibu wao kama mamlaka ya kwanza ya nidhamu kwa mwalimu kwa mujibu wa sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu namba 25 ya mwaka 2015.
Alisema mwalimu atakapoandikiwa kibali cha kustaafu, TSC pamoja na mfuko wa mifuko ya hifadhi ya jamii wanajikita zaidi kuangalia taarifa za mwalimu alizojaza awali, wakati anaanza ajira yake na sio kutegemea taarifa za stakabadhi ya mishahara peke yake.
Rutahindurwa aliweka bayana kuwa yapo madhara kwa mwalimu ambaye muda wake wa kustaafu utafika lakini akaendelea kuwepo kazini kwa kuwa wakati wa kuchukua mafao yake, atakatwa mishahara yote aliyolipwa kwa kipindi chote alichofanya kazi baada ya muda wake wa halali wa kustaafu kupita.
“Naomba muwaeleze walimu wote katika shule zenu kuwa utakapoandikiwa kibali cha kustaafu sisi tunaangalia zaidi taarifa zako ulizojaza wakati unaajiriwa na kibainika umedanganya utachukuliwa hatua kwa kuwa umemwibia mwajiri,” alisisitiza.
Alisema TSC ina taarifa zote za walimu walizojaza wakati wa kuajiriwa, hivyo kwa waalimu wote ambao hawakumbuki taarifa zao wawasiliane na ofisi za tume ya utumishi wa walimu katika wilaya zao ili kupata uhakika wa tarehe zao za kustaafu.
Alieleza kuwa kuna wakati walimu walitakiwa kupeleka taarifa zao za kiutumishi kwa waajiri wao, lakini baadhi yao walipeleka taarifa tofauti na zile walizojaza kwenye mikataba ya kazi, wakati wa kuanza ajira.
“Kuna baadhi ya waalimu wanajifanya hawakumbuki walizaliwa mwaka gani wakati walijaza mikataba wakati wanaanza ajira na wengi wao wamebadilisha taarifa zao na kujipunguzia umri jambo ambalo ni kinyume na taratibu na sharia,” alisema.
Katibu huyo aliwaeleza waalimu kuwa kwa mujibu wa sheria ya utumishi wa walimu namba 25 ya mwaka 2015, wao ndio mamlaka ya kwanza ya nidhamu kwa walimu.
Hivyo, wanapaswa kuwashauri na kuwaelimisha waalimu juu ya kanuni na taratibu za kiutumishi badala ya kukaa na kusubiri wafanye makosa ili wawachukuliwe hatua.
Walimu walionesha kupokea maelekezo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi ili kuondoa usumbufu kwa mwalimu pale anafuatilia masuala yake ya mafao mara baada ya kustaafu.
Walimu hao wametoa pongezi kwa katibu wa TSC kwa jitihada kubwa anazofanya katika kuhakikisha mashauri ya walimu yanafanyiwa kazi na maamuzi yanatolewa kwa muda muafaka.
Mbali na walimu, serikali imekuwa ikisisitiza juu ya watumishi wengine ambao wako kazini huku wakijua kwamba walipunguza umri wao ili wasifikie mapema muda wa kustaafu, ikisema kwamba ni kosa la jinai na kuwa baada ya kufuatilia waliopatikana na vyeti vya kufoji, pia ina mpango wa kugeukia hata waliopunguza umri kazini.



Read also-: