-->

Profesa Hubert Kairuki kuenziwa kwa shughuli za kijamii

Shirika la Afya na Elimu la Kairuki (KHEN) katika kumuenzi muasisi wa taasisi hiyo, marehemu, Profesa Hubert Kairuki itafanya mambo mbalimbali ya kijamii ikiwamo kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa kituo cha kusaidia watu wenye matatizo ya kupata watoto.
Akizungumza leo Jumapili Februari 4 kwenye mkutano na waandishi wa habari, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki Profesa Charles Mgone amesema taasisi hiyo ya Kairuki itaweka jiwe hilo kwaajili ya kuanza ujenzi wa kituo kitakachotoa huduma kwa wanawake ambao hawana uwezo wa kushika mimba na wanaume ambao hawawezi kutungisha mimba kwa njia ya kawaida.
"Kwa sasa kuna changamoto kubwa ya wanawake kushika ujauzito kwa njia ya kawaida na hata wanaume, katika kumuenzi muasisi wetu tutaweka jiwe hilo kesho eneo la Bunju" amesema.
Amesema kituo hicho kikikamilika kitakuwa msaada kwa familia ambazo hazijabahatika kupata watoto kwa njia za kawaida kwani kitahusika na upandikizaji wa mbegu na ushauri kwa wenye matatizo hayo.
"Mchoro kwaajili ya ujenzi wa kituo upo katika hatua za mwisho na tayari taasisi hiyo imeandaa wataalamu ambao watatoa huduma hizo pindi kitakapokamilika" amesema.
Profesa Mgone amesema mbali na hilo pia wataanzisha kliniki ya mama, baba na mtoto, watatoa huduma za afya bure kwa wananchi wote kuanzia kesho hadi sita Februari mwaka huu.
‘’Tutakuwa na shughuli nyingi kwa kipindi cha siku tatu kuanzia keshom tutakuwa na uchangiaji wa damu, tutakuwa na mashindano ya kitaalamu baina ya wanafunzi wa shule ya uuguzi Kairuki na chuo kikuu cha Kairuki hayo yote yatafanyika Bunju"amesema.
Amesema watakuwa na upimaji wa shinikizo la damu, uwiano wa urefu na unene na kutoa ushauri.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Hospitali ya Kairuki, Dk. Asser Mchomvu akimwelezea marehemu Kairuki aliyefariki Februeri 6,1999 ,amesema alikuwa na uzalendo na nchi yake alipenda watanzania wapate huduma bora za afya ndiyo maana aliamua kuanzisha huduma za afya binafsi lengo ni kusaidia msongamano hospitali za umma.
"Tungeweza kumuenzi kwa kuimba nyimbo za huzuni lakini tukaona hapana ngoja tumuenzi kwa kufanya mambo ambayo alipenda kufanya wakati wa uhai wake" amesema Dk Mchomvu

Read also-: