-->

Mahitaji ya vyuo, kiwanda cha nyama Simiyu


https://tpc.googlesyndication.com/simgad/4375051796857061867

UJENZI wa vyuo mkoani Simiyu ni moja ya fursa kuu kati ya 14 za uwekezaji zinazopatikana Simiyu kutokana na utafiti wa kisayansi uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Masuala ya Kiuchumi na Kijamii (ESRF).
Watafiti hao wanasema kwa sasa kinachohitajika kwa haraka ni chuo cha kilimo na ufugaji ambacho wanashauri kijengwe katika wilaya ya Busega na chuo cha teknolojia ya viwanda, wakishauri kijengwe Bariadi palipo makao makuu ya mkoa.
Kwa mujibu wa ESRF, kutokana na mkakati wa kufanya mabadiliko makubwa katika kilimo na viwanda, Simiyu inahitaji vyuo hivyo vya kilimo na viwanda vitakavyozalisha nguvu kazi itakayohitajika sana katika kuubadilisha mkoa katika maeneo hayo.
Kwamba kutokana na ongezeko la haraka la watu la asilimia 2.8 na hatua ya serikali kutoa elimu bure, Simiyu haiwezi kukwepa kuhitaji vyuo vya ufundi vya kutosha na hivyo ni wakati mwafaka sasa kwa watu kuchangamkia fursa hizo.
Kiwanda cha nyama Fursa nyingine kwa mujibu wa ESRF ambayo wawekezaji wanapaswa kuimulika ni ujenzi wa kiwanda cha nyama mkoani Simiyu, hatua itakayotoa soko la uhakika la wafugaji wa ng’ombe na hivyo pia kuwafanya wafuge kabiashara zaidi.
Simiyu kwa sasa inakadiriwa kuwa na zaidi ya ng’ombe milioni 1.5, wengi wakiwa aina ya Zebu ambapo asilimia 90 wanafugwa na wananchi lakini bado wanatoa mazao kidogo.
Kiwanda hiki cha nyama kinashauriwa kwenda sambamba na uwepo wa kiwanda au viwanda vya kuzalisha vyakula vinavyosaidia kunenepesha ng’ombe sambamba na kuwepo kwa machinjio ya kisasa. ESRF wanasema ongezeko la ukuaji wa miji katika mkoa wa Simiyu bila shaka litakwenda sambamba na ongezeko la mahitaji ya nyama.
Halikadhalika, watafiti hao wanasema kuna soko la kutosha la nyama katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na hata nje ya Jumuiya hiyo.
Ujenzi wa nyumba nafuu Kwa mujibu wa ESRF, Simiyu pia inahitaju nyumba za kisasa lakini zenye bei nafuu ambazo wananchi wengi wanaweza kuzinunua kwa mtindo ambao wajenzi wataona unawezekana.
Watafiti hao wanasema kwa sasa asilimia 40 ya wakazi wote wa Simiyu ni vijana walio chini ya umri wa miaka 30 ambao katika mwongo mmoja ujao wataanzisha familia na kuhitaji nyumba za kuishi.
“Simiyu ni mkoa mpya, hivyo kutakuwa na ongezeko la watu wanaohamia katika mkoa huu kwa ajili ya kufanya kazi, kufanya biashara au kutafuta fursa hizi na zile. Hawa wote watahitaji nyumba,” inasomeka ripoti ya awali ESRF ikiwa na kichwa cha habari, ‘Muongozo wa Uwekezaji Mkoani Simiyu.’
Taasisi za kiserikali kama Shirika la Kiuchumi la Jeshi la Kujenga Taifa (Suma JKT) na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) wanahimizwa na watafiti kuchangamkia fursa hizo adhimu bila kusahau makampuni binafsi ya ujenzi.
Mbali na hizo fursa zilizojadiliwa hapo juu, fursa zingine ambazo tumeshaziangalia kwa kina ni uzalishaji wa pamba yenye kiwango bora na uchimbaji wa mabwawa sambamba na kuendesha skimu za umwagiliaji.
Katika mfululizo huu tuliangalia pia ushauri wa kutenga maeneo au miji, mawili maalumu kwa ajili ya viwanda, maduka na huduma nyingine za kifedha na ujenzi wa viwanda vya kisasa vya kuchambua pamba na vya nguo.
Tutaendelea kujadili fursa zingine zilizobaki kwa kina katika jarida la Uchumi Jumanne wiki ijayo, ambazo ni fursa za huduma za ugani kwa wanyama (veterinary services), kiwanda cha ngozi na viwanda vya kuzalisha bidhaa za ngozi, Fursa nyingine zinazopatikana Simiyu tutakazoziangalia kwa kina ni viwanda vya kusindika mafuta ya kula yatokanayo na mbegu, viwanda vya maziwa na mazao yake, uwindaji wa kitalii, bandari, usafiri na michezo ya majini katika wilaya ya Busega.
Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, ameshaweka wazi kwamba yeyote mwenye kutaka kuwekeza mradi utakaokuwa na manufaa kwa wana-Simiyu ikiwemo kutoa ajira kwa vijana, atapewa ardhi bure.
Na tayari Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN), inayochapisha magazeti ya Daily News, Habari- Leo na SpotiLeo, iliandaa Jukwaa la Biashara lililoketi Februari 13 na kushirikisha wadau muhimu wa maendeleo.
Wakati TSN ikifanya kazi ya kupaza sauti ili wananchi wajue “Simiyu kunani”, wadau wa jukwaa, hususani taasisi za fedha, TIB na NMB zilionesha namna watu wanavyoweza kuzitumia kuwekeza Simiyu huku Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ikieleza namna ya kuhakikisha kodi zinalipwa.
Na katika kuwafanya wana- Simiyu sasa walale na kufikiria kibiashara, jukwaa pia lilishirika Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka. Kiuchumi (NEEC)

Read also-: